You are currently viewing Dkt Samia: Tanzania inalenga kuzalisha Megawati 10,000 ifikapo 2050

Dkt Samia: Tanzania inalenga kuzalisha Megawati 10,000 ifikapo 2050

Na Mwandishi Wetu

Rais wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan amesema Tanzania imejiwekea lengo la kuzalisha megawati 10,000 za umeme ifikapo mwaka 2050, ikiwa ni sehemu ya maono ya maendeleo ya taifa na mkakati wa kuimarisha usalama wa nishati nchini.

Akizungumza katika Mkutano wa Ubunifu wa Nishati ya Nyuklia Afrika (NEISA 2026) mjini Kigali, Rwanda, Dkt Samia amesema kwa sasa Tanzania ina uwezo wa kuzalisha zaidi ya megawati 4,500 huku mahitaji yakitarajiwa kufikia megawati 7,000 ifikapo mwaka 2030.

Amesema Tanzania inaendelea kuangalia matumizi ya nishati ya nyuklia kama sehemu ya kuongeza vyanzo vya umeme na kuhakikisha ukuaji endelevu wa uchumi pamoja na usalama wa nishati wa muda mrefu.

Aidha, Dkt Samia amesema Tanzania tayari imeandaa ramani ya maendeleo ya nishati ya nyuklia inayokwenda sambamba na viwango vya Shirika la Kimataifa la Nishati ya Atomiki (IAEA), pamoja na kuanzisha taasisi maalumu ya kuratibu maandalizi ya mradi huo.

Pia, amesema Tanzania inaendelea kufuatilia teknolojia mpya za vinu vidogo vya nyuklia ambavyo vinaonekana kuwa suluhisho rafiki kwa nchi zinazoendelea zinazohitaji umeme wa uhakika kwa ajili ya viwanda na uchumi.