You are currently viewing Ethiopia yazindua bwawa kubwa zaidi la kuzalisha umeme Afrika

Ethiopia yazindua bwawa kubwa zaidi la kuzalisha umeme Afrika

Ethiopia imezindua rasmi Bwawa la Grand Ethiopian Renaissance (GERD), mradi mkubwa zaidi wa kuzalisha umeme barani Afrika.

Sherehe ya uzinduzi ilifanyika juzi Jumanne karibu na bwawa hilo katika eneo la kaskazini magharibi la Benishangul-Gumuz kusherehekea kukamilika rasmi kwa mradi huo.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wakuu wa Ethiopia, viongozi wa Afrika na wawakilishi kutoka Umoja wa Afrika na mashirika mengine ya kimataifa, akiwemo Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika Mahmoud Ali Youssouf, Rais wa Kenya William Ruto, Rais wa Djibouti Ismail Omar Guelleh na Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir.

Ujenzi wa mradi huu wa kuzalisha umeme wa megawati 5,150 ulianza mwaka 2011 katika Mto Blue Nile karibu na mpaka wa Sudan.

Akihutubia hafla hiyo, Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed alisisitiza uwezo wa bwawa hilo kuimarisha uchumi wa taifa kwa kutoa nishati ya uhakika kwa viwanda, kuboresha maisha ya wananchi na kuendeleza ushirikiano wa kikanda wa nishati.

Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed akizungumza katika hafla iliyofanyika karibu na Bwawa la Grand Ethiopian Renaissance (GERD) katika eneo la kaskazini magharibi la Benishangul-Gumuz, Ethiopia

“Hongera kwa Wethiopia wote, walio nyumbani na walioko ughaibuni, pamoja na marafiki wetu duniani kote, kwa uzinduzi huu wa kihistoria wa Bwawa la Grand Ethiopian Renaissance,” alisema.

Mradi huo, wenye uwezo wa kuhifadhi jumla ya mita za ujazo bilioni 74 za maji, umekuwa chanzo cha mvutano mrefu kati ya nchi tatu zinazotegemea Mto Nile: Ethiopia, Misri na Sudan.

Wakati Cairo na Khartoum zikiogopa bwawa hilo litapunguza mgao wao wa maji, Addis Ababa imesisitiza kwamba mradi huo hautadhuru nchi zilizoko chini ya mto.

“Ni waumini thabiti wa maendeleo ya pamoja,” alisema Abiy, akithibitisha tena dhamira ya Ethiopia ya kufanikisha ukuaji bila kudhoofisha maslahi ya majirani zake.

Mto Blue Nile, unaojulikana nchini Ethiopia kama Mto Abay, unatokea katika Ziwa Tana takribani kilomita 570 kaskazini mwa Addis Ababa na ni mojawapo ya mito mikuu miwili inayounda Mto Nile.

Leave a Reply