Waziri Mkuu, Mwigulu Nchemba, amesema Serikali imebaini na kuwakamata baadhi ya watu wanaowalipa na kuwaandikisha vijana wa Kitanzania ili kuwapeleka barabarani (kuandamana).
Mwigulu, ameeleza hayo leo, Jumamosi Julai 27, 2026 alipozungumza na wananchi wa Ikungi mkoani Singida, wakati wa ziara yake.
“Haya mambo hatuwezi kuyaruhusu, kuna kijana mmoja kutoka wilayani moja, kila mwezi analipwa Sh3 milioni kwa ajili ya kushawishi vijana waingie barabarani.
“Anafanya hayo yote wale wanaomlipa wana faida gani na nchi yetu, wanataka kunufaikaje na hayo anayoyafanya? Haya mambo lazima tuwaambie ukweli Watanzania kuna watu wana nia mbaya na nchi yetu,” amesema.
Pia, amesema kuna mwingine analipwa Sh5 milioni kwa mwezi, baada ya kuulizwa akaeleza kuwa katumwa na watu ambao tayari imebainika wanakoishi.
“Ametoa siri nyingi tu, wale wanaomtuma na wenyewe wanafugwa na kulipwa kwa ajili ya shughuli ya namna hii. Ndio maana kila siku wanaweka mikakati ya uhalifu, wanapanga siku ya matukio ya kukusanya watu,” amesema Mwigulu.
Amesisitiza Serikali haitamchekea yeyote anayetaka kuleta machafuko nchini, akivitaka vyombo vya ulinzi na usalama kuwa imara wakati wote.
