Wakati Watanzania wakiuanza mwaka mpya, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan amesema mwaka 2026 Serikali imejipanga kujenga umoja wa kitaifa nchini.
Dkt Samia ameeleza hayo leo Desemba 31,2025 katika hotuba yake kwa Watanzania ya kuufunga mwaka 2025 na kuukaribisha mwaka mpya wa 2026.Mkuu huyo wa nchi, amezungumza moja kwa moja na Watanzania akiwa Ikulu ya ndogo ya Tunguu, mkoa wa Kusini Unguja, Mjini Zanzibar.
“Tunapouanza mwaka 2026, Serikali imejipanga kujenga umoja wa kitaifa nchini. Hatua za kuunda Tume ya maridhiano zimeanza kuchukuliwa,” amesema Dkt Samia nakuongeza kuwa:
“Serikali itashirikiana na wadau wote katika kukubaliana kuhusu muundo wa Tume, aina ya wajumbe, majukumu yao, na muda wa kazi wa Tume hiyo,” amesema mkuu huyo wa nchi.
Amefafanua kuwa katika kuelekea kutekeleza jukumu hilo la kuijenga Tanzania, Dkt Samia amewataka Watanzania kutokubali kugawanyika kwa tofauti za kiitikadi au mtazamano utakaosababisha kupoteza malengo ya maendeleo na ustawi wa Taifa.
“Sote tunafahamu kuwa, tofauti ni sehemu ya demokrasia, lakini zisitumike kuligawa Taifa la Tanzania.
“Narudia kusema kuwa, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni moja tu; ndani ya Jamhuri hiyo kuna Watanzania waliojengwa na itikadi ya kuamini amani, umoja na mshikamano hujenga Uzalendo na ndio virutubisho vinavyotuletea maendeleo endelevu na ustawi wa Watanzania,”
