Kwa mara nyengine, Cuba imekosa umeme nchi nzima kutokana na uchakavu wa miundombinu na uhaba wa mafuta kwenye mitambo ya nishati katika taifa hilo la Karibiki.
Tukio hilo la jana Jumatano ni la pili kwa mwaka huu, likitanguliwa na matukio ya aina hiyo mwaka jana.
Wizara ya Nishati na Madini imeandika kupitia mtandao wa kijamii wa X kwamba kukatika huko kwa umeme kulitokana na kuharibika kwa mojawapo ya kinu kikubwa kabisa cha umeme nchini humo.
Waziri Mkuu Manuel Marrero ametembelea kinu hicho na amewaomba raia kuendelea kuwa na imani na serikali wakati ikiendelea kulishughulikia tatizo hilo.
Vikwazo vya kiuchumi vya Marekani, vinavyolenga kuilazimisha Cuba ibadilishe mfumo wake wa kisiasa, vimelifanya taifa hilo kuingia kwenye hali mbaya ya kiuchumi na mzozo wa nishati.
Vikwazo hivyo vimeikosesha Havana fedha za kigeni za kununulia mafuta ama vifaa kwa ajili ya mitambo yake, mengi yao ikiwa na zaidi ya miaka 30 bila matengenezo.